Breaking




Friday 6 October 2017

CHAMA CHA WAMILIKI WA BUNDUKI MAREKANI KIMEKUJA NA HILI HUHUSU MAPINDUZI YA SHERIA ZA BUNDUKI.

Sungo blog

Chama cha taifa cha wamiliki wa bunduki Marekani (NRA) kimeonekana kubadilisha msimamo wake na kuunga mkono udhibiti wa vifaa ambavyo hutumiwa kuimarisha uwezo wa bunduki.

Kifaa kama hicho kilitumiwa na mwanamume aliyewaua watu 50 kwenye tamasha mjini Las Vegas.

Kundi hilo limesema: "Vifaa hivyo ambavyo huwezesha bunduki ambazo zina uwezo fulani wa kufyatua risasi mfululizo kuwa bunduki kamili za kufyatua risasi mfululizo kwa kujiendesha yenyewe."

Chama cha Republican kimesema kwamba kitajadili uwezekano wa kupiga marufuku kifaa hicho kwa jina 'bump-stock' ambacho huondoa haja ya mtu anayetumia bunduki isiyo na uwezo kamili wa kufyatua risasi mfululizo kutumia bega lake kuidhibiti bunduki wakati wa kufyatua risasi.

Wabunge wanapanga kuandaa vikao na kujadili mswada wa kupiga marufuku kifaa hicho.

Alhamisi, NRA walitoa wito kwa wadhibiti wa bunduki "kuchunguza mara moja iwapo vifaa hivyo vinafuata sheria za serikali ya taifa."

Rais Donald Trump baadaye aliwaambia wanahabari kwamba utawala wale utafikiria uwezekano wa kuzipiga marufuku "muda mfupi ujao."

"Baada ya shambulio hilo la kinyama Las Vegas, Wamarekani wanatafuta majibu kuhusu jinsi ya kuzuia maafa kama haya siku za usoni," wakuu wa NRA Wayne LaPierre na Chris Cox waliandika kwenye taarifa.

Hata hivyo, wamewakosoa wanasiasa ambao wanatetea udhibiti zaidi wa bunduki, wakisema kwamba "kupiga marufuku raia wanaotii sheria kumiliki bunduki kwa sababu ya kitendo cha kihalifu cha mwendawazimu hakutazuia mashambulio kama haya siku za usoni."

Taarifa hiyo ndiyo ya kwanza kutoka wka chama hicho tangu shambulio hilo la Jumapili Las Vegas ambapo watu 58 waliuawa na wengine zaidi ya 500 kujeruhiwa.

NRA hata hivyo wamesema vifaa hivyo viliidhinishwa na Shirika la Kudhibiti Silaha, Pombe na Tumbaku wakati wa utawala wa Rais Obama.

Msemaji wa White House Sarah Sanders, akizungumza na wanahabari baada ya taarifa ya NRA kutolewa, amesema: "Wanachama wa vyama vyote viwili na mashirika mengi wote wanapanga kuangalia upya vifaa hivyo. Tunakaribisha hilo na tungependa kuwa sehemu ya mazungumzo yanayoendelea."

Kwenye taarifa yao, NRA walihimiza Bunge la Congress kupitisha pendekezo lao la kuhakikisha haki za kumiliki silaha zinatekelezwa kote nchini humo.

Chama hicho kinataka wamiliki wa silaha wenye leseni za kubeba silaha wakiwa wamezificha kwenye jimbo moja waruhusiwe kuingia kwenye majimbo mengine bila kujali iwapo sheria za umiliki wa silaha huko ni tofauti.

Mswada wa kupiga marufuku vifaa hivyo vya kuimarisha uwezo wa bunduki uliwasilishwa kwenye bunge la Seneti Marekani siku ya Jumatano na seneta wa chama cha Democratic kutoka California Dianne Feinstein.

Mswada mwingine wa aina hiyo unaowasilishwa na chama cha Republican huenda ukawasilishwa bungeni muda wowote kuanza siasa, seneta wa chama cha Republican kutoka Florida Carlos Curbelo amewaambia wanahabari.

Stephen Paddock, mshambuliaji aliyewaua watu wengi Las Vegas, alikuwa ameweka vifaa hivyo kwenye bunduki 12 alizozitumia kwenye shambulio hilo.

Vifaa hivyo hugharimu chini ya $200 (£150) na huwezesha bunduki kufyatua risasi hadi 100 katika sekunde saba pekee, kwa mujibu wa tangazo la moja ya kampuni zinazouza vifaa hivyo.

Slide Fire, moja ya kampuni zinazouza vifaa hivyo, imesema bidhaa walizounda zimenunuliwa zote baada ya wateja kufika kwa wingi kufuatia shambulio hilo la Las Vegas.

No comments:

Post a Comment